WASIFU WA TVLA

1. UTANGULIZI  

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) ni Wakala ya Serikali chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliyoanzishwa kwa Sheria ya Wakala za Serikali Cap. 245 (iliyofanyiwa marekebisho Mwaka 2009) na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali la tarehe 9 Machi 2012. Wakala ilizinduliwa rasmi tarehe 11 Julai, 2012 na Katibu Mkuu Kiongozi. Wakala hii ilitokana na kuunganishwa kwa iliyokuwa Maabara Kuu ya Mifugo (CVL), Vituo vya Kanda vya Uchunguzi na Utambuzi wa Magonjwa ya Mifugo (VICs), Taasisi ya Utafiti wa Ndorobo (TTRI) Tanga na Kituo cha Utafiti wa Ndorobo (TTRC) Kigoma.

 

2. DIRA YA WAKALA

Dira ya Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania ni kuwa kituo cha umahiri katika kutoa huduma bora za maabara za Veterinari, bidhaa bora za Veterinari na kufanya utafiti juu ya vimelea vya magonjwa ya wanyama na wadudu waenezao magonjwa hayo ndani na nje ya Tanzania.

 

3. DHAMIRA YA WAKALA

Kutoa mchango stahiki katika kuimarisha uzalishaji endelevu wa sekta ya Mifugo, usalama wa chakula na kuchangia kwenye uchumi wa Taifa kupitia utoaji wa huduma bora za uchunguzi na utambuzi wa magonjwa ya mifugo kwa gharama nafuu, huduma bora za uchambuzi wa kiveterinari, uzalishaji na usambazaji wa bidhaa bora za veterinari na kufanya tafiti juu ya magonjwa ya wanyama na wadudu waenezao magonjwa

 

4. MAJUKUMU YA WAKALA

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) katika kutekeleza kazi zake kutokana na malengo ya kuundwa kwake ina majukumu kadhaa inayoyatekeleza ambayo ni pamoja na;

  1. Uchunguzi na utambuzi wa Magonjwa ya Wanyama;
  2. Uzalishaji na usambazaji wa Chanjo za Mifugo;
  3. Uhakiki wa Ubora wa Vyakula vya Mifugo;
  4. Usajili na uthibiti wa ubora wa viuatilifu vya Mifugo;
  5. Utafiti wa magonjwa ya Wanyama na wadudu waenezao magonjwa hayo; na
  6. Kutoa huduma za ushauri na mafunzo.

 

MUUNDO WA WAKALA

Wakala ina Muundo uliopitishwa kwa mujibu wa sheria

 

TVLA Organization Structure

 

 

SISI NI NANI

Wakala wa Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) ni Wakala Mtendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (MLF), iliyoanzishwa chini ya Sheria ya Wakala wa Utendaji Sura ya 245 (Toleo Lililorekebishwa; R.E 2009), iliyotangazwa kwenye Gazeti la Serikali namba 74 la nyongeza ya Machi 9, 2012. Nambari 8 na kutangazwa na Katibu Mkuu Kiongozi tarehe 11 Julai, 2012.

Wakala ilianzishwa kufanya kazi na kufikia malengo yafuatayo:-

  1. Kutengeneza na kuuza vifurushi vya kiteknolojia na biolojia zinazofaa.
  2. Kuanzisha mifumo ya Usimamizi.
  3. Kufanya na kuimarisha huduma za uchunguzi na uchunguzi.
  4. Kuboresha miundombinu na vifaa.
  5. Kuimarisha mifumo ya usimamizi wa Fedha na Rasilimali Watu
  6. Imarisha mpangilio wa kitaasisi.
  7. Kushughulikia masuala mtambuka

 

Kazi Zetu:

Jukumu kubwa la TVLA ni kutekeleza lengo la kuanzisha mfumo wa maabara ya mifugo kama ilivyoainishwa katika sera ya taifa ya mifugo (2006). Majukumu na majukumu ni:-

1. Kufanya uchunguzi na uchunguzi wa magonjwa ya wanyama na wadudu.

2. Kutengeneza na kuzalisha chanjo na biolojia nyinginezo.

3. Kupima na kutathmini biolojia, kemikali za ethno-mifugo na maabara.

4. Kuchambua usalama wa malisho ya mifugo;

5. Kuthibitisha vipimo na viwango vya magonjwa ya wanyama na uchunguzi wa kimaabara

6. Kutoa huduma za rufaa za maabara ya mifugo na magonjwa yanayoenezwa na wadudu na wadudu kwa Tanzania na kanda ya SADC kwa magonjwa maalum.

7. Kuanzisha na kudumisha msingi wa data juu ya magonjwa ya wanyama na wadudu.

8. Kuendeleza na kuboresha vifurushi vya teknolojia.

9. Kusimamia maabara za mifugo.

10. Kuthibitisha viuatilifu vya mifugo.

11. Kuthibitisha vipodozi vya mifugo, dawa na vifaa.

 

Uchunguzi na Utambuzi wa Magonjwa ya Wanyama

Wakala kupitia maabara zake hupokea sampuli za wanyama mbalimbali kwa ajili ya kufanya uchunguzi na utambuzi wa magonjwa ya mifugo. Njia mbalimbali za uchunguzi zinazotumika ni pamoja na kuchunguza vimelea vya magonjwa kwa kutumia hadubini, kuchunguza viashiria vya uwepo wa kinga dhidi ya kimelea kwenye damu kwa kutumia ELISA na kipimo cha juu kabisa cha uchunguzi wa aina ya kimelea kwa kutumia vinasaba yaani PCR.

 Chanjo zinazozalishwa na Wakala ni pamoja na: -

  1. Chanjo stahimilivu joto ya kukinga kuku dhidi ya ugonjwa wa Mdondo (TEMEVAC);
  2.  Chanjo ya ugonjwa wa Kimeta (ANTHRAX VACCINE);
  3.  Chanjo ya ugonjwa wa Chambavu (BLACKQUARTER);
  4.  Chanjo ya Homa ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP);
  5.  Chanjo ya ugonjwa wa Kutupa Mimba (S19);
  6.  Chanjo mchanganyiko wa Kimeta na Chambavu (TECOBLAX); na
  7. Chanjo ya Homa ya Mapafu ya Mbuzi (CAPRIVAC).

 

Uhakiki wa ubora wa vyakula vya mifugo

Wakala inatambuliwa na Sheria ya Maeneo ya Malisho na Rasilimali za Vyakula Vya Wanyama sura Na. 180 ya Mwaka 2010 na Kanuni yake ya Mwaka 2012 kuwa mchambuzi wa ubora wa vyakula vya mifugo kitaifa. Wakala ina maabara yenye vifaa vya kisasa na wataalamu wabobezi katika Kupima na kuthibitisha ubora wa vyakula vya mifugo ikiwemo.

  1. Viwango vya viini lishe kama vile nishati na protini;
  2. Viwango cha amino asidi muhimu;
  3. Aina na kiwango cha madini;
  4. Ubora wa soya kwa ajili ya kutengenezea vyakula vya mifugo;
  5. Kiwango cha mchanga katika malighafi ya kutengenezea vyakula vya mifugo kama vile dagaa n.k.

 

Usajili na uthibiti wa ubora wa viuatilifu vya Mifugo

Wakala imekabidhiwa jukumu la kusajili na kuthibiti matumizi ya dawa za kuogeshea mifugo, jukumu ambalo kwa muda mrefu lilikuwa likifanywa na iliyokuwa ikijulikana kama Taasisi ya Utafiti wa Viwatilifu (TPRI). Kupitia maabara yake ya Kemia iliyoko katika Maabara Kuu ya Mifugo, Wakala hupokea sampuli za viuatilifu vinazoingizwa na waagizaji (wafanyabiashara) binafsi toka nje ya nchi ili kupima ubora wake. Aidha, maabara pia hupokea sampuli za maji ya josho ili kupima nguvu ya dawa katika maji hayo na kuzishauri Kamati za Majosho juu ya matumizi sahihi ya viuatilifu wanavyovitumia.

 

Utafiti wa magonjwa ya Wanyama na wadudu waenezao magonjwa hayo

Wakala ina wataalamu wa mifugo ambao hufanya tafiti mbalimbali zinazolenga kutafuta njia mbalimbali za kupambana na kudhibiti magonjwa ya mifugo na wadudu waenezao magonjwa hayo.

 

Huduma za Ushauri

kama ilivyo kwa wataalamu wengine, wataalamu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania - TVLA, hutoa huduma za ushauri mbalimbali kwa wananchi kulingana na majukumu ya taasisi kama vile ushauri kuhusu magonjwa ya Wanyama na wadudu waenezao magonjwa hayo, matumizi sahihi ya Chanjo za Mifugo, Ubora wa Vyakula vya Mifugo pamoja na matumizi sahihi ya viuatilifu vya Mifugo. Pamoja na hilo, Wakala pia inashiriki katika kutoa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wanaosoma taaluma ya ufundi sanifu maabara na fani nyingine za kisayansi kutoka vyuo mbalimbali hapa nchini na nje ya nchi. Pia, Wanafunzi wa shahada na shahada za juu (Uzamili na Uzamivu) hutumia maabara za Wakala katika kufanya tafiti zao.

 

UTAFITI WA NJIA ZA KUDHIBITI MBUNG’O (NDOROBO)

Wakala kupitia kituo chake cha utafiti wa wadudu na magonjwa wayaenezayo cha VVBD Tanga hutoa huduma ya kuangamiza mbung’o katika maeneo yaliyo jirani na mbuga za wanyama. Mbung’o ni wadudu wanaoeneza ugonjwa wa Nagana kwa mifugo na Malale kwa binadamu. Kupitia tafiti za kuangamiza mbung’o, teknolojia mbalimbali zimeibuliwa ikiwa ni pamoja na matumizi ya mitego ya vitambaa inayonasa mbung’o pamoja na teknolojia ya vifukuzi na vivutizi.

 

UTEKELEZAJI WA MFUMO WA UTHIBITI WA VIWANGO VYA UBORA

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania ina kitengo kinachosimamia mfumo wa uthibiti wa viwango vya ubora katika kazi zake. Utekelezaji wa mfumo huo umepelekea maabara za TVLA kupata Ithibati (accreditation) ya kimataifa   kwa vipimo kumi (10) vya kimaabara kutoka shirika la viwango vya ukaguzi kwa nchi za kusini mwa Afrika yaani Southern African Development Community Accreditation Services (SADCAS) kwa Ithibati nambari VET 007 ya ISO/IEC 17025:2022.  Vipimo hivyo ni pamoja na:

  1. HA/HI kwa ugonjwa wa Mdondo;
  2. Fluorescent Antibody Test (FAT) kwa ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa;
  3. PPR ELISA kwa ugonjwa wa Sotoka ya Mbuzi na Kondoo;
  4. PPR RT PCR kwa ugonjwa wa Sotoka ya Mbuzi na Kondoo;
  5. NSP FMD ELISA kwa ugonjwa wa Miguu na Midomo;
  6. FMD PCR kwa ugonjwa wa Miguu na Midomo;
  7. Real Time PCR kwa ugonjwa wa Kutupa Mimba;
  8. Rose Bengal Plate Test kwa ugonjwa wa Kutupa Mimba;
  9. CBPP Competitive ELISA kwa Homa ya Mapafu ya Ng’ombe; na
  10. Brucellosis Indirect ELISA kwa ugonjwa wa Kutupa Mimba.